WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA AKOSHWA NA UTENDAJI KAZI WA OFISI YA MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI.

Imewekwa: 25 Nov, 2025
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA AKOSHWA NA UTENDAJI KAZI WA OFISI YA MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI.

Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Dkt. Juma Zuberi Homera ametembelea Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na kufanya mazungumzo na Menejimenti ya Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali tarehe 25 Novemba, 2025.

Mhe. Dkt. Homera amepongeza Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kufanya kazi kwa ushirikiano na kwa ufanisi mkubwa.

”Niipongeze Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kufanya kazi kwa ushirikiano, na sasa hivi mikataba ikija hapa inafanyiwa kazi nakukamilika kwa haraka nawapongeza sana” amesema Dkt. Homera

Vilevile  Mhe. Waziri wa Katiba na Sheria amempongeza Mwanasheria Mkuu wa Serikali na timu yake kwa kazi kubwa wanayoifanya.

”Lakini pia napenda kumpongeza Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Timu yake, kwa kazi kubwa wanayoifanya, sisi kama Wizara tunatambua mchango wake” amesema Dkt. Homera

Aidha, Mhe. Waziri akizungumzia suala zima la kutoa huduma bora za Kisheria kwa wananchi , alisisitiza kuwa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ina nafasi ya kipekee katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora za kisheria na kusisitiza,
”Sisi Viongozi tuna mchango mkubwa wa kuleta hali ya unafuu wa maisha ya Watanzania" 

Awali, akimkaribisha  Mhe. Waziri, Naibu Waziri wa Katiba na Sheria  Mhe. Zainab Athman Katimba aliipongeza Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kufanya  kazi  kwa ubora na ufanisi.

Aidha, Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali  Mhe. Samwel M. Maneno akitoa Taarifa kuhusu Majukumu na Mafanikio ya Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali  alimshukuru Mhe. Waziri  kwa ziara hiyo na kumuelezea Mafunzo mbalimbali yanayotolewa kwa watumishi yakiwa na lengo la kuwaimarisha na kuwaongezea ujuzi utakaowasaidia katika kuboresha utendaji kazi wao.

”Katika kipindi cha Julai, 2025 hadi Septemba, 2025 jumla ya watumishi 117 walipatiwa mafunzo mbalimbali” amesema Mhe. Maneno.

Katika kuhakikisha Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali inafikisha huduma za kisheria karibu zaidi kwa wananchi,  Mhe. Naibu Mwanasheria Mkuu alitaja Ofisi za Mwanasheria Mkuu wa Serikali zilizoko katika mikoa ambazo zinaendelea kutoa huduma kwa wananchi wa mikoa hiyo .

Katika Ziara hiyo Mhe. Waziri aliambatana pia  na Naibu Katibu Mkuu Dkt. Franklin Jasson Rwezimula na Mkurugenzi Msaidizi Huduma za Kisheria kwa Umma Bw. Abdulrahman M. Msham.