WAOMBA OMMS KUANDAA MAFUNZO ENDELEVU KUHUSU MIRADI YA PPP

Imewekwa: 06 Jul, 2023
WAOMBA OMMS KUANDAA MAFUNZO ENDELEVU KUHUSU MIRADI YA PPP

 

 Dodoma-Naibu Mwanasheria Mkuu  Serikali ya  Mapinduzi  Zanzibar  Shaaban Ramadhan Abdalla  ameelezea kuridhishwa kwake na  mafunzo waliyopewa ya kuwajengea uelewa kuhusu miradi ya Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi ( PPP).

Amesema  mafunzo hayo yamekuwa na umuhimu hasa kwa upande wa Zanzibar ambako  serikali ya awamu ya nane imeamua kufungua milango ya uwekezaji.

“mafunzo  haya yamekuwa ya muhimu  sana kwetu sote  na hasa sisi  kutoka Ofisi ya Mwanasheria Mkuu  Zanzibar ambako Serikali ya Awamu ya Nane imefungua milango kwa wawekezaji kutoka ndani na nje ya nchi,  na ndiyo maana tumekuja washiriki 20  kwenye mafunzo hayo ambao wanatoka   Divisheni ya Mikataba”.

Naibu Mwanasheria Mkuu  Shaaban  Ramadhan Abdalla  ameyasema hayo wakati wa uhitimishaji  wa mafunzo ya siku  nne  ya kuwajengea uwezo na uelewa kuhusu miradi ya PPP mafunzo ambayo  yameratibiwa na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kushirikiana na kwa ufadhili wa Taasisi ya  Kimataifa ya  African Legal Support Facility (ALSF).

Mafunzo hayo yamefanyika katika Ukumbi wa Mikutano  ulipo katika Hoteli ya Dodoma  jijini Dodoma. Jumla ya washiriki 60 kutoka Taasisi mbalimbali wakiwamo  Mawakili wa Serikali  kutoka Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

Pamoja na  kuelezea kuridhishwa  na mafunzo hayo ambayo watoa mafunzo walikuwa ni wataalamu kutoka Taasisi ya Pinsent Massons Bw. John Woolley na Bw.  Jonathan  Hart,Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali  amesema  Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali  Zanzibar  itaendelea  kushirikiana kwa karibu   na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Akizungumza kwa niaba ya  washiriki wa mafunzo hayo Bi Nzeyimana Dyegula kutoka Shirika la Reli Tanzania ( TRC) pamoja na kupongeza kuwapo kwa mafunzo hayo ameomba na kushauri Ofisi ya Mwanasheria  Mkuu wa Serikali  kuendelea kuratibu mafunzo ya aina hiyo kwa kushirikiana na  wadau wake.

Akasema  mafunzo ya  uandaaji,  utekelezaji,  usimamia na ufuatiliaji  wa miradi ya PPP ni  muhimu sana  na yanatakiwa kuwa endelevu hasa kutokana na miradi hiyo kuwa na changamoto nyingi.

“Kwa niaba ya  washiriki wenzangu  kwanza  nisema  tunaishukurua Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali  kwa  uratibu wa mafunzo haya kwa kushirikiana na ALSF, mimi  binafasi  nimekuwa nikishughulikia miradi hii ya PPP kwa Zaidi ya miaka sita sasa,  lakini  nikiri  kwamba bado nakumbana na changamoto nyingi  kwa hiyo  tunapopatiwa mafunzo  kama haya siyo tu  tunajifunza mambo mapya lakini pia  tunajifunza na namna ya kukabiliana na changamoto” akasema  Bi.Dyegula

Aidha amesema kutoka na  unyeti wa miradi ya PPP mafunzo yakuwajengea uwezo  wataalamu pamoja na  Mawakili wa Serikali ni muhimu sana na kwamba yeye binafsi amefurahishwa na mchanganyiko wa wataalamu waliohudhuria mafunzo haya.

“Kwa mara ya kwanza  nimehudhuria mafunzo haya kuhusu miradi hii ya PPP pasipokutana na  mtu ninaye mfahamu tofauti  na huku nyuma semina au mafunzo ya aina hii  utakuta watu ni wale wale lakini hapa ni tofauti na hii inatupatia  fursa ya kujifunza na kubadilishana  uelewa kwa upana zaidi.

Aidha  washiriki hao wamesema mafunzo  haya  yamekuwa mazuri zaidi  kwa sababu wakufunzi walikuwa ni wanasheria wenzao na hivyo  kuongea lugha  wanayoelewana na yalikuwa shirikishi.

Haya ni Mafunzo ya  awamu ya pili kuratibiwa na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kushirikiana na ALFS  ya  mafunzo ya awamu ya kwanza  yalihusu masuala ya  madini,  gesi na mafuta.

Imeandaliwa na  Kitengo cha Mawasiliano

6/7/2023