TANZANIA YATAKA USHIRIKIANO KUTOKOMEZA UVUVI HARAMU

Imewekwa: 17 Oct, 2023
TANZANIA  YATAKA USHIRIKIANO KUTOKOMEZA   UVUVI HARAMU

Na  Mwandishi  Maalum

Tanzania  imezitaka  nchi wanachama wa  Taasisi ya Mashauriano  ya Sheria ya Nchi za Asia na Afrika (AALCO) kushirikiana katika  kumaliza  tatizo la  uvuvi haramu.

Nchi wanachama wa AALCO wanakutana katika mkutano wao  wa  61 unaofanyika   katika  ukumbi wa  Mikutano  wa  Bali Nusa Dua, Mjini  Bali,   Indonesia. Naibu  Mwanasheria  Mkuu wa Serikali  Mhe. Balozi Kennedy Gaston  ameongoza Ujumbe wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali  katika   Mkutano huo.

 Katika  wasilisho  hilo, Tanzania imeeleza kuwa tatizo la  uvumi haramu  linaziathiri sana nchi za Visiwa Vidogo  na Nchi za Maziwa  Makuu na hivyo ushirikiano wa kulimaliza tatizo hilo ni jambo linalotaka  ushirikiano wa dhati  wa  nchi wanachama wa Taasisi hiyo.  

Pamoja na  tatizo  hilo la uvuvi haramu,  Tanzania  pia imesisitia  haja na umuhimu wa kulinda  raslimali  za Bahari kwa  ustawi  na maendeleo ya nchi wanachama wa AALCO na dunia kwa ujumla.

 Katika  hatua nyingine, Tanzania  imeelezea utayari wake wa  kushirikiana na Nchi Wanachama katika kubadilishana uzoefu na kujengeana uwezo katika masuala ya sheria za bahari na uchumi wa bluu pamoja na sheria za biashara na uwekezaji kwa maendeleo  endelevu ya dunia.

Katika  Mkutano huo wa wiki moja,  nchi wanachama zinajadili masuala mtambuka ya sheria za kimataifa hususani katika sheria za Bahari na uchumi wa bluu.

Aidha,  nchi hizo pia, zinajadiliana   jinsi ya kupambana na uvuvi haramu, sheria za biashara na uwekezaji na utatuzi wa migogoro  katika  vituo vya usuluhishi wa  migogoro  vya  Kimataifa.

 Wanachama pia  watajadiliana  kuhusu na  masuala  yenye manufaa kwa AALCO ambayo yapo kwenye agenda ya Kamisheni ya Sheria za Kimataifa ya Umoja wa Mataifa (International Law Commission).

Mkutano huo pia  utajadiri  suala  la  uvunjifu wa sheria za kimataifa kwenye maeneo ya Palestina; sheria za utwaaji mali zilizoibiwa  , mazingira na maendeleo endelevu.

 Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali Balozi Gaston katika mkutano huo  ameambatana na Mawakili wa Serikali waandamizi Hassan Nkya kutoka Idara ya Uandishi wa Sheria na Felista Lelo kutoka Idara ya Mikataba.

Maafisa  hao  wawili  wamekuwa wakishiriki    mikutano ya kitaalamu ya pembezoni (side events).

 Mkutano huu pia ulihudhuriwa na ujumbe kutoka Wizara ya Katiba na Sheria ambao uliongozwa na Naibu Katibu Mkuu Dkt. Khatibu Kazungu.

AALCO inawanachama  47.Tanzania ilijiunga mwaka  1973

17/10/2023