MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI ASHIRIKI ZIARA YA TUME YA UTUMISHI WA MAHAKAMA

Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mhe. Hamza S. Johari ameshiriki katika ziara ya Tume ya Utumishi wa Mahakama inayoendelea katika Mikoa ya Rukwa na Katavi ambapo tarehe 27 Mei, 2025 amehudhuria kikao cha Tume ya Utumishi wa Mahakama pamoja na Watumishi wa Mahakama wa Mkoa wa Katavi kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Katavi.
Mwanasheria Mkuu wa Serikali ni mjumbe wa Tume ya Utumishi wa Mahakama kwa mujibu wa Ibara ya 112 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Katika ziara hiyo Mwanasheria Mkuu wa Serikali ameongozana na Mwenyekiti wa Tume hiyo Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma.
Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Mahakama, Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma ambaye ameongoza kikao hicho amemshukuru Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kuwa kiungo muhimu baina ya Serikali na Mahakama katika masuala mbalimbali ikiwemo Utungaji wa Sheria ambazo zimerahisisha utendaji kazi katika Mahakama.
“Tunamshukuru Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kutengeneza na kuboresha sheria mbalimbali ambazo zimerahisisha utendaji wa haki kwa urahisi na kupunguza mlundikano wa mashauri”. Amesema Prof. Juma
Aidha, Mhe. Jaji Mkuu amempongeza Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kushiriki katika shughuli mbalimbali za maboresho ya Mahakama na kuipa kipaumbele ziara hiyo ya Tume ya Utumishi wa Mahakama licha ya kuwa na ratiba ngumu zinazomkabili
“Tunakupongeza Mhe. Johari kwa ushiriki wako katika masuala mbalimbali yanayoihusu Mahakama pamoja na kuipa umuhimu ziara hii pamoja na kukabiliwa na ratiba ngumu ikiwemo vikao vya Bunge linaloendelea”. Amesema Jaji Mkuu.
Mwanasheria Mkuu wa Serikali akizungumza katika kikao hicho amefurahishwa na hatua zilizofikiwa na Mahakama katika kuboresha miundo mbinu yake hivyo kurahisisha utendaji kazi wa Mahakama.
"Niipongeze sana Tume ya Mahakama kwa kuboresha miundombinu ya mahakama katika mikoa mbalimbali nchini hivyo kurahisisha utoaji wa haki kwa wananchi". Amesema Mwanasheria Mkuu wa Serikali.
Ziara hiyo ya Tume ya Utumishi wa Mahakama katika Mikoa ya Katavi na Rukwa imeanza tarehe 27 na inatarajia kukamilika tarehe 30 Mei, 2025 na inalenga kuitambulisha Tume katika mikoa hiyo, kusikiliza changamoto za watumishi wa Mahakama na kuwakumbusha wajibu wao wa kutenda haki, pamoja na kukagua miradi ya maboresho ya Mahakama inayoendelea kutekelezwa.