MCHAKATO WA UREKEBU WA SHERIA KUU KUKAMILIKA MARCHI 2023.

Imewekwa: 05 Mar, 2023
MCHAKATO WA UREKEBU WA SHERIA KUU KUKAMILIKA MARCHI 2023.

MCHAKATO WA UREKEBU WA SHERIA KUU KUKAMILIKA MARCHI 2023.

Na Mwandishi Maalumu

Iringa

 Mwandishi Mkuu wa Sheria   Bw. Onorius Njole  amewataka   washiriki wa kikao kazi ambacho kimeanza mchakato wa mwisho wa  kukamilisha zoezi la urekebu wa  Sheria Kuu kuhakikisha   wanaukamilisha mchakato huo kwa wakati na kwa viwango  vya hali  ya juu.

Ameyasema hayo  leo  jumamosi(March 4,2023) wakati akifungua rasmi   shughuli za kikao kazi hicho  kinachofanyika katika Hotel ya  Mt.Royal Villa Mkoani Iringa, kikao ambacho washiriki wake ni  kutoka Divisheni ya Uandishi wa Sheria Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

Bw. Njore amewataka Mawakili hao wa Serikali  ambao miongoni mwao ni  waandishi wakuu wa sheria,  waandishi washeria waadamizi,  mawakili wa serikali na warekebu wa sheria kuhakikisha kuwa  katika umoja wao siyo tu wanakuwa na uelewa wa pamoja  wa ukamilishaji wa  mchakato mzima wa urekebu wa sheria lakini  wanatoa sheria  zitakazokuwa na viwango na ubora wa hali ya juu.

“ Niwasihi sana ushiriki wenu katika mchakato  huu mzima wa urekebu wa sheria  si jambo dogo, ni ushiriki muhimu sana kwa mustakabali wa tasna ya  sheria  katika nchi yetu, lakini kupitia kwenu  nchi yetu itapata sheria   ambazo siyo tu zitakuwa katika juzuu moja bali pia zenye  viwango vya hali ya juu viwango ambavyo vimetokana na  umakini na  uadilifu wenu”.   Akasisiza Mwandishi Mkuu wa Sheria.

Pamoja na  kuwasisitiza washiriki wa Kikao kazi hicho kuhakikisha sheria  zilizofanyiwa  urekebo zinakuwa   za  viwango.

Amewasihi  wataalamu hao kwamba zoezi la urekebu wa sheria zote kuu takribani 446 linatakiwa kukamilika  mwezi huu wa Marchi 2023.

Katika kikao  kazi  cha wataalamu hao wa uandishi  na urekebu wa sheria  ambao wote ni kutoka Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali  wakiwamo  Mawakili wa Serikali ambao wameajiriwa hivi karibuni  wamepitia   na kujadili kipengele kwa kipengele  cha muongozo wa  mambo muhimu ya kuzingatia wakati wa  mchakato mzima  wa urekebu wa sheria na hasa katika uandishi wa  sheria hizo.

Mapendekezo ya muongozo  wa  mambo muhimu ya kuzingatia katika mchakato mzima wa urekebu wa sheria  uliwasilishwa na Mwandishi Mwandamizi  wa Sheria  Wakili wa Serikali  Bwa. Shabani Kagunga.

Muongozo huo utawasaidia  wataalamu hao    kuwa na uelewa wa pamoja, uelewa ambao  mwishoni  utapelekea  sheria zote ambazo zitakuwa zimefanyika urekebu kuwa na mwonekano unaofanana.

Pamoja na  kupitia na kujadili muongozo huo,  watakuwa na  kazi kubwa ya  kuzipita sheria zote ambazo zimefanyiwa urekebu kwa kuzingatia   muongozo huo lakini pia  watakuwa na jukumu la  kuandaa nyaraka mbalimbali  ukiwamo muswada  unaohusiana na mchakato  mzima wa zoezi hilo  la urekebu wa sheria.  

Mwandishi wa Habari hizi na ambaye amehudhuria  kwa mara ya kwanza  shughuli za urekebu wa  sheria ameshuhudia namna ambavyo wataalamu hao  walivyokuwa wakijadiliana na kupingana kwa hoja hadi kufikia muafaka wa nini  walichoamini kinapaswa kuwa  kifungu sahihi  kuwepo ndani ya muongozo huo ili   yawe sehemu ya   muongozo wa kushughulikia masuala mbalimbali kabla ya kuandaliwa muswada wa  marekebisho ya sheria zilizorekebiwa.

Kwa  upande wake  Mwandishi wa Sheria Mkuu mstaafu  Bi. Grace Mfinanga anayeshiriki zoezi hili  na kuchangia uzoefu wake, pamoja na  mambo mengine, amewataka mawakili hao wa serikali wanaoshiriki jukumu hilo kuonyesha uadilifu na uaminifu wa hali ya juu wakati wote wa kutekeleza jukumu hilo.

Akasema  uandishi wa sheria na urekebu wa sheria siyo jukumu la mchezo na kwamba linahitaji  usiri wa hali  ya juu sana na kuwataka kujisikia Fahari  kuwa sehemu ya zoezi hilo.

Pamoja na kuzipitia  tena sheria hizo kuu,  kikosi kazi  hicho pia kitakuwa na  jukumu kama ilivyoelezwa wali  la  kuandaa nyaraka na  matangazo mbalimbali yatakayotolewa  sambamba na  toleo la urekebu wa sheria pamoja na  muswada wa marekebisho ya sheria ambazo zitahusika katika toleo la sheria zilizorekebiwa la mwaka 2023.

 

Zoezi la urekebu wa sheria kuu na ambalo limekuwa likitekelezwa na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali   kupitia Divisheni  yake ya Uandishi wa Sheria na  kwa kushirikiana na  wadau mbalimbali  lilianza  mwaka 2020 kwa hatua za awali  na linagharimiwa na  Serikali  ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa asilimia  mia moja.

Imeandaliwa na  Kitengo cha  Mawasiliano

4/3/2023