AG FELESHI ATOA WITO KWA TAASISI ZA KISHERIA ZA SERIKALI KUJIFANYIA TATHMINI YA UTEKELEZAJI WA MAJUKUMU YAO

Imewekwa: 06 Jun, 2023
AG FELESHI ATOA WITO KWA   TAASISI ZA KISHERIA  ZA  SERIKALI  KUJIFANYIA  TATHMINI YA  UTEKELEZAJI WA MAJUKUMU YAO

DODOMA-Mwanasheria Mkuu wa Serikali  Mhe. Jaji Dkt. Elizer Mbuki Feleshi amezitaka   Taasisi za Kisheriaza Serikali   kujifanyia  tathimini ya utekelezaji wa majukumu yao na kutoa mapendekezo  ya changamoto wanazokabiliana  nazo ili  zifanyiwe  kazi.

Ametoa agizo  hilo   siku ya  Jumatatu ( June 5/2023 )wakati akitoa salamu za pongezi kwa Ofisi ya Wakili  Mkuu wa Serikali  kwa kufikisha  miaka mitano  tangu kuundwa kwake mwaka 2018. Na  mgeni  rasmi katika maadhimisho hayo alikuwa  Waziri Mkuu  Mhe.  Kassim Majaliwa.

Maadhimisho hayo  yanakwenda sambamba na mafunzo ya kuwajengea uwezo na uelewa   Mawakili  wa Serikali  kuhusu  masuala mbalimbali yakiwamo ya uendeshaji wa kesi za madai,  majadiliano na usuluhishi.

Mhe Mwanasheria Mkuu wa Serikali  pamoja na  kuzitaka Taasisi za Kisheria za Serikali  kuiga   mfano huo  wa Ofisi ya Wakili  Mkuu wa Serikali wa kujitathmini  amewataka pia  Mawakili wa Serikali nao kujifanyia tathmini.

Amekasema “ Ogopa sana tu ambaye kila kukicha ni kama jana, hakuna mabadiliko wakati nyakati zinabadilika hata magonjwa  yanabadilika”.

Akasema yeye kama kiongozi Mkuu wa Mawakili  wa Serikali  takribani 3,449 moja ya jukumu lake la msingi ni kuhakikisha mawakili hao wa serikali  wanakuwa wenye  weledi, ubora na uwezo wa kutekeleza majukumu  mtambuka.

Akisisitiza kuhusu nafasi yake ya    Uongozi  kwa Mawakili  wote wa Serikali  amezikumbusha Taasisi za  Kisheria za  Serikali  na Mawakili  wote wa Serikali  kukumbuka  kuwa wanatekelekeza majukumu yao kwa niaba yake.

“ Mhe. Mgeni Rasmi, Mimi ndiye  kiongozi wa  Mawakili  wote wa Serikali  ambao hadi  June 3 tulikuwa  3450  lakini  kwa sasa tupo  3449 baada ya  Wakili Mmoja kufariki June 3 2023, sasa  wakati nikiwapongeza Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali kwa  kuadhimisha miaka mitano  tangu kuanzishwa kwake ikiwa ni pamoja na kujitafanyia tathmini,   walipotoka  walipo na wanapokwenda,  nipende  kuwakumbusha kwamba utekelezaji wa majukumu yao lazima utokane na uzingatie  maelekezo yangu” akasisitiza na kuongeza.

“Ofisi ya  Wakili   Mkuu wa Serikali nafikiri kuna  jambo linalofanyika na vilevile Ofisi ya Taifa ya Mashtaka. Hamuwezi kufanya  jambo lolote nisifahamu na taasisi nyingine, kwa sababu kwa mujibu wa sharia  hawa wote wanaleta taarifa  zao kwangu na kupokea maelekezo kutoka kwangu”

Akasema  angependa kutumia muda huo wa kutoa salamu zake kumwomba Wakili  Mkuu wa Serikali kuwa hatekelezi  majukumu yake bila kupata  maelekezo kutoka kwa mwanasheria Mkuu wa Serikali.

“Ni muhimu sana Wakili Mkuu wa Serikali uwafundishe hasa  Mawakili  wapya wasije wakatekeleza majukumu yao bila  maelekezo ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali “. Akasisitiza Mhe. Feleshi.

Akizungumzia zaidi kuhusu  miaka mitano ya Ofisi ya  Wakili Mkuu wa Serikali,  Mhe. Feleshi amebainisha kwamba  kama kuna mtu  mwenye furaha basi ni yeye.

Akasema  furaha yake hiyo  inatokana na kushuhudia maboresho   makubwa ambayo yamefanyika katika  Tasnia ya Sheria hususani Taasisi za kisheria za Serikali   maboresho ambayo  amesema yameongeza tija na ufanisi mkubwa  katika utoaji wa haki lakini pia katika kuisaidia serikali katika utekelezaji wa majukumu yake ya kuwaletea wananchi maendeleo na ustawi wao.

“ kama ni  jeshini  basi mimi  ningekuwa   Jenerali  kutokana na kushuhudia  mengi na  kushiriki katika   maboresho na mageuzi katika tasnia  ya sharia hapa nchini. Nimeshuhudia  na ninaushuhuda mkubwa wa   tulikotoka  tulipo na  tunapoelekea basi niwaombe wenzagu tuyautumie maadhimisho haya  pamoja na mafunzo kujijengea msingi bora na imara ya utekelezaji wa majukumu yetu” akasisitiza Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

Akawakumbusha Mawakili wa Serikali  kauli ya  Mhe. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alivyowaita  Mawakili  hao  Septemba mwaka jana kuwa na Jeshi la kulinda uchumi wa Nchi  kwa kutumia kalamu zao na taaluma yao.

Imeandaliwa na  Kitengo  cha Mawasiliano

5/6/2022