“TOENI ELIMU YA SHERIA ZA UCHAGUZI KWA WANANCHI” – NAIBU MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI

Imewekwa: 27 Jun, 2025
“TOENI ELIMU YA SHERIA ZA UCHAGUZI KWA WANANCHI” – NAIBU MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI

Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Samwel M. Maneno, amekutana na kufanya mazungumzo na ujumbe kutoka Kampuni ya The Guardian Limited, wachapishaji wa magazeti ya The Guardian na Nipashe, katika Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mtumba Jijini Dodoma, tarehe 26 Juni, 2025.

Mazungumzo hayo yalilenga kuimarisha mahusiano kati ya taasisi za kiserikali na vyombo vya habari pamoja na kujadiliana juu ya Taasisi hizo zinavyoweza kushirikiana katika kuwahabarisha wananchi majukumu na mafanikio mbalimbali yaliyofikiwa katika Sekta ya Sheria.

Akizungumza katika kikao hicho Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali, amesema kuwa ni muhimu kwa vyombo vya habari kutoa elimu ya Sheria ya Uchaguzi kwa wananchi ili waweze kuielewa.  

“Niwaombe muendelee kutoa elimu ya sheria mbalimbali na katika kipindi hiki tulichopo toeni elimu ya kutosha kuhusu Sheria za Uchaguzi ili wananchi waweze kuielewa." Amesema Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

Aidha, Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali ameeleza kuwa Ofisi yake iko tayari muda wowote kushirikiana na vyombo vya habari ili kuweza kutoa taarifa sahihi kwa wananchi, aidha amesema Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali inatambua mchango mkubwa wa vyombo vya habari katika kukuza demokrasia, kutoa elimu kwa umma, na kushirikiana na taasisi za umma katika kuhimiza utawala bora.

“Tunatambua nafasi ya vyombo vya habari katika kutoa elimu kwa wananchi, Ofisi yetu iko wazi muda wote kushirikiana nanyi katika kuhakikisha kuwa wananchi wanapata taarifa sahihi kupitia vyombo vya habari”. Ameeleza Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

Kwa upande wake, Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa The Guardian Limited Bw. Jackson Paul ameishukuru Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali  kwa mapokezi mazuri waliyoyapata na ziara yao imekuwa na mafanikio makubwa kwakuwa wamejifunza mambo mengi ya kisheria huku akiahidi  wataendeleza ushirikiano huo kwa kuuhabarisha umma juu ya masuala mbalimbali ya kisheria yanayotekelezwa na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

“Tunawashukuru sana kwa kutupokea, kipekee nikushukuru Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kutenga muda wako na kuzungumza nasi, tumejifunza mambo mengi ambayo tutaenda kuyafanyia kazi.” Amesema Bw. Jackson 

Ujumbe kutoka Kampuni ya The Guardian Limited uliotembelea Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali uliongozwa na Naibu Mkurugenzi Mtendaji Bw. Jackson Paul, Mhariri wa Habari Bi. Salome Kitomari, Mkuu wa Masoko Kanda ya Kati Bw. Raymond Mushi, Msimamizi wa Mkoa wa Dodoma Bi. Linda Samwel, Afisa Masoko Bi. Sekela Kilembe  na Mwandishi wa Gazeti la Nipashe Bw. Peter  Mkwavila.

Aidha, katika hicho kilichoongozwa na Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mhe. Samwel M. Maneno Kilihudhuriwa pia na Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali Bi. Leila Muhaji na Wakili wa Serikali Bw. Hassan Nkya.